Sunday 18 January 2015

KWA NINI USILE TENA MKATE MWEUPE KUANZIA LEO?


Mkate ndiyo chakula kikuu cha kila siku cha familia nyingi duniani, hasa sehemu za mijini na ndiyo chakula kinachotumika na watu wa rika zote, wakubwa kwa wadogo, lakini ni wangapi tunajua kuwa mkate mweupe, ambao ndiyo chaguo namba moja la familia nyingi, ni hatari kwa afya zetu?
Kuna msemo maarufu wa Kiingereza kuhusu mkate mweupe usemao: The Whiter the Bread, the Quicker You are Dead! kwa tafsiri isiyo rasmi, msemo huu unamaanisha kuwa ‘kadiri unavyopenda kula mkate mweupe, ndivyo utakavyokufa haraka!’ Amini, usiamini, mkate mweupe siyo mzuri kwa afya yako!
Inawezekana kabisa habari hii isikufurahishe, lakini kama kweli unataka kuboresha afya yako, unapambana na suala la kupunguza unene, unataka kujiepusha na hatari ya kupatwa na ugonjwa wa kisukari (Type II), ugonjwa wa moyo au saratani ya tumbo, basi huna budi ya kuachana na mkate mweupe.
Kama tulivyosisitiza kila mara katika makala zetu nyingi za nyuma kuwa vyakula vyote vitokanavyo na nafaka zilizokobolewa vina hasara zaidi kiafya kuliko faida, mkate mweupe nao ni miongoni mwa vyakula hivyo.

KWA NINI USILE MKATE MWEUPE?
Kama ujuavyo, mkate unatengenezwa kutokana na ngano na mkate mweupe unatokana na unga wa ngano iliyokobolewa na kuondolewa virutubisho vyake muhimu vya asili ambavyo huwa muhimu katika uimarishaji wa mfumo wa usagaji na umeng’enyaji chakula tumboni (Digestive system and metabolism).
Ili unga uwe mweupe, ngano baada ya kukobolewa husafishwa kwa mashine maalumu kwa kutumia kemikali na joto kali, kitendo ambacho huondoa kabisa virutubisho vinavyoweza kuwemo kwenye nafaka na hivyo kuiacha punje ya ngano ikiwa nyeupe na kubaki makapi.
Makapi hayo, baadaye husagwa na kuwa unga safi na mweupe ambao hutayarishwa kabla ya kutengenezwa mkate kwa kupitia hatua mbalimbali, ikiwemo hatua ya kuwekewa hamira ili uumuke, kuongezewa sukari pamoja na chumvi ili kuongeza ladha.

MADHARA YANAYOWEZA KUKUPATA KWA KULA MKATE MWEUPE
Madhara ya kwanza unayoweza kuyapata kwa kupenda sana kula mkate mweupe ni ugonjwa wa kisukari. Utafiti unaonesha kuwa mkate au chakula chochote kilichotengenezwa kutokana na unga mweupe kina kiasi kingi cha wanga ambao husababisha kuongezeka sukari mwilini.
Madhara mengine yatokanayo na mkate mweupe ni kuongezeka kwa lehemu (bad LDL cholesterol) kwenye damu, hali ambayo inaweza kusababisha presha au magonjwa ya moyo yatokanayo na kusinyaa au kuziba kwa mishipa ya damu.
Madhara hayajaishia hapo, mengine yanayoweza kukupata ni tatizo la ukosefu wa choo kwa muda mrefu. Mkate mweupe huchangia kuvuruga mfumo wa umeng’enyaji wa chakula tumboni (metabolism). Mwili unapokuwa hauna virutubisho vya kutosha, usagaji na uondoaji wa sumu mwilini huwa wa shida na uchafu unaporundikana tumboni kwa muda mrefu bila kutoka, husababisha kansa ya tumbo!
ULE NINI BADALA YA MKATE?
Kuna aina nyingine ya mkate ambayo ndiyo unayopaswa kula, mkate huo ni BROWN BREAD au MKATE MWEUSI kama unavyojulikana na wengine. Mkate huu hutengenezwa kutokana na ngano isiyokobolewa hivyo kuwa na virutubisho vyake asilia vinavyohitajika mwilini na kuwa na faida zitakazokuepusha na kupatwa na madhara yaliyotajwa hapo juu. Mkate huu hauna sukari wala chumvi, hivyo kuwa bora zaidi kwa afya yako. Kama kweli unajijali, utaacha kula mkate mweupe na kuanza kula huu mweusi leo!

0 comments:

Post a Comment