Wednesday 7 May 2014

(FALLOPIAN TUBES) FAHAMU KUHUSU MIRIJA YA MAYAI

MIRIJA ya mayai ipo miwili kwa mwanamke upande wa kulia na kushoto wa kizazi na kazi kubwa ni kuruhusu yai kupita toka katika kifuko cha mayai kwenda kwenye mrija.


Mwishoni mwa mrija kuna vidole vinavyoitwa ‘fimbriae’ na katikati ya mrija ni sehemu pana  iitwayo ‘Ampulla’ ambapo ndipo mimba inatungwa.
Sehemu nyembamba na ndogo ya mrija ipo pale mrija unapojikita kwenye kizazi, inaitwa ‘isthmus’.


Mrija wa mayai 
unatabaka nne, kuna tabaka la nje kabisa, la kati, la ndani na ndani kabisa ambazo zina majina yake ya kitaalamu. 


Ndani ya mrija wa mayai kuna vinyweleo viitwavyo ‘Cillia’ ambavyo kazi yake kubwa ni kusukuma yai na majimaji mengine yasiyohitajika humo.
Mirija imejishika vizuri katika kizazi na sehemu ya pembeni katika eneo la nyonga.
 
Kazi ya mrija wa mayai
Yai linapoanza kuendelezwa hadi kupevuka linakuwa limezungushiwa ukuta laini ili kulilinda, ukuta huu uitwao ‘Ovarian follicle’ yai linapokomaa, kifuko hicho hupasuka na kuruhusu yai litoke kisha kuchukuliwa na kidole ‘fimbriae’ na kulisafirisha hadi ndani ya mrija kwenye sehemu iitwayo Ampulla ambapo ndipo hukutana na mbegu ya kiume na kutungisha mimba.


Baada ya siku tano tangu mimba kutungwa, mimba hiyo inakuwa imeshasafiri na kujikita katika kizazi. Kama mimba haitatungwa, basi yai hilo litatoka na damu ya hedhi. Kama mimba itatungwa kama kawaida kwenye mrija na itashindwa kusafiri na kuendelea kukua kwenye mrija, mimba hiyo 

haitaendelea na ndipo tunasema mwanamke ana mimba nje ya kizazi ‘Ectopic Pregnancy’ na mrija unaweza kupasuka na hali ya mama ikawa mbaya. Hili tutakuja kuona katika makala zijazo.
Kwa kawaida tangu mtoto anapoumbwa tumboni mwa mama anakuwa na viungo sawa, vya kike na kiume.


Kwa mtoto wa kike kuna mirija inajitokeza miwili, kulia na kushoto iitwayo ‘Mullerian ducts’ ambayo inakuja kuwa mirija ya mayai, kwa mwanaume kuna ‘Wolffian ducts’ ambayo inakuja kuwa mirija ya kusafirisha mbegu.

Matatizo katika mirija
Matatizo katika mirija husababishwa na maambukizi yaitwayo kitaalamu ‘Salpingitis’. Maambukizi haya yanaweza kuathiri mrija mmoja au yote miwili. Chanzo kikuu cha maambukizi haya ni maambukizi katika viungo vya uzazi ‘ PID’ ambayo tumeshaona katika makala zilizopita.


Matatizo mengine yanayoweza kuathiri mirija ni hali iitwayo ‘Endometriosis’ ambapo katika hali isiyo ya kawaida, tabaka la ndani la kizazi huwa nje ya kizazi.


Ugonjwa wa PID 
zaidi husababishwa na bakteria wa aina ya ‘Chlamydia Trachomatis’. 
Maambukizi ya muda mrefu husababisha mirija kuziba hivyo kumfanya mwanamke awe mgumba au apate mimba nje ya kizazi.
Mrija wa mayai pia unaweza kupata saratani au kansa, kansa hiyo pia inaweza kuwa au kusambaa katika vifuko vya mayai.

Dalili za matatizo ya mirija
Mwanamke hulalamika maumivu ya tumbo chini ya kitovu yanayosambaa kulia na kushoto, kushindwa kupata ujauzito kwa kipindi cha zaidi ya mwaka mmoja.

Uchunguzi na tibaVipimo mbalimbali hufanyika kama Ultrasound kuangalia maambukizi ya ndani ya kizazi, vipimo vingine vya kuchunguza mirija ni kama vile HSG, Laparascopy na Dye au Gycosy. Matibabu ya mirija iliyoziba huitwa ‘Tubal insulfflation’ 
kutegemea na kiwango cha uzibaji baada ya  kufanya mojawapo ya vipimo hapo juu na kuthibitisha mirija imeziba. 
Uzibuaji wa mirija baada ya vipimo hufanyika baada ya kuhakikisha  hakuna maambukizi ndani ya kizazi.

Ushauri
Wahi hospitali kwa uchunguzi wa kina. Muone daktari wa kinamama katika hospitali za wilaya na mikoa kwa uchunguzi wa kina. Epuka maambukizi ya kizazi na utibiwe mapema, hatari ya yote ni kupoteza uwezo wa kuzaa.

0 comments:

Post a Comment