Wednesday 7 May 2014

UYOGA: KINGA BORA DHIDI YA SARATANI


VIRUTUBISHO 
maalum vinavyopatikana kwenye uyoga, vimevuta hisia za watafiti kwa zaidi ya miaka 20 sasa ili kupata uhakika kwamba mboga hii ina 
uwezo mkubwa wa kutoa kinga kwa mwili wa mwanadamu dhidi ya ugonjwa wa saratani, ikiwemo ya matiti.

Uyoga una vitamini 
na aina nyingi za madini. Virutubisho vilivyothibitishwa kuwemo kwenye uyoga ni pamoja na Vitamin B2, B3, B5, B6, B Complex pamoja na madini ya Potasiamu na ‘phosphorus’. Virutubisho hivyo ni muhimu 

kwenye mwili wa binadamu katika kutoa na kuimarisha kinga ya kupambana na ‘wavamizi’ maradhi.

Aidha, 
inaelezwa kuwa uyoga ni chanzo kingine kizuri sana cha madini ya chuma (iron) na kopa ambayo yanahusika kwa kiasi kikubwa na uwezeshaji wa usambaza wa hewa ya oksijeni mwilini. Kupatikana kwa madini ya chuma na kopa kwenye uyago ni jambo la kipekee ambalo linafanya mmea huo kuwa tofauti na muhimu.


Zikifafanuliwa nguvu za uyoga 
(Mashrooms) kwa mapana, inaelezwa kuwa Vitamin B2 inayopatikana kwenye uyoga, ni tiba tosha kwa watu wanaosumbuliwa na ugonjwa wa kichwa unaojulikana kama ‘kipanda uso’. Kiasi kidogo cha uyoga utakachokula kitapunguza kasi ya kuumwa kichwa hicho.

Vilevile Vitamin B
inasifika kwa uwezo wake wa kuzuia uchovu wa mwili (fatique) na akili hasa wakati wa kazi nyingi. Vitamin B3 husaidia kupunguza kiwango cha mafuta mabaya ya Kolestrol mwilini, wakati Vitamin B6 yenyewe huondoa hatari ya mtu kupatwa na kiharusi au moyo kusimama ghafla (Heart Attack).

Kama faida zote za kiafya 
zilizo orodheshwa hapo juu zinazopatikana kwenye uyoga hazikutosha, basi kuna faida nyingine ambayo inatokana na madini aina ya Zinc yanayopatikana kwa wingi kwenye mboga hii. Zinc ina faida nyingi sana mwilini na miongoni mwa faida hizo ni uimarishaji wa kinga ya mwili (Immune System).

Zinc si muhimu 
tu kwa uimarishaji wa kinga mwilini, bali pia kwa uponyaji wa haraka wa vidonda mwilini. Vilevile mboga hii inasaidia sana ukuaji mzuri wa seli za mwili, huimarisha kiwango cha sukari mwilini na kukufanya kusikia ladha na harufu ya vyakula na vitu vingine ipasavyo.

Kwa ujumla uyoga 
ni mboga muhimu na inapaswa kuliwa na kila mtu anayejali afya yake kutokana na faida zinazopatikana humo. Kuanzia leo, jaribu kuweka uyoga katika orodha ya mboga unazonunua kila wiki kwa ajili ya familia yako.


Bila shaka kwa wakazi 
wa miji midogo na vijijini, mboga hii hupatikana kwa wingi wakati wa mvua na kwa miji mikubwa kama Dar es Salaam, uyoga unaweza kupatikana kwenye masoko maalum kama, Kariakoo, Kisutu na ‘super market’ mbalimbali.

0 comments:

Post a Comment