Tuesday 12 August 2014

UPUNGUFU WA DAMU KWA MJAMZITO



Upungufu wa damu (anaemia) hutafsiriwa kama kupungua kwa kiwango cha hemoglobin katika damu chini ya kiwango kinachokubalika kiafya.
Kiwango cha kawaida cha hemoglobin (Hb) katika mwili wa binadamu ni kati ya gramu 12 mpaka 14 kwa kila mililita ya damu.
Hata hivyo, Shirika la Afya Duniani (WHO) linatambua kiwango cha mpaka 11gm/mililita kuwa cha kawaida kwa mama mjamzito.
Hivyo basi mjamzito mwenye kiwango chochote cha hemoglobin chini ya 11 gm/mililita hutafsiriwa kuwa na upungufu wa damu. Hata hivyo, nchi nyingi hasa zinazoendelea hutambua kiwango cha mpaka gramu 10 kwa mililita kuwa ni upungufu wa damu kwa mjamzito.
Kwa mjamzito anayehudhuria kliniki kwa mara ya kwanza, upungufu wa damu kipindi cha ujauzito humaanisha kiwango cha hemoglobin chini ya 11.0 g/dL, na mimba inapofikisha wiki 28 upungufu wa damu hutambuliwa iwapo hemoglobin itashuka na kuwa chini ya 10.5 g/dL.
Kwa kuzingatia hilo, mama mjamzito hushauriwa kupima wingi wa damu siku anapohudhuria kliniki kwa mara ya kwanza na pindi mimba inapofikisha wiki 28.
Upungufu wa damu unaweza kugawanywa katika viwango vikuu vinne, yaani upungufu wa damu wa kawaida (mild anaemia) ambao ni kati ya 9-11 gm/ml, upungufu wa damu wa kati (moderate anaemia) ambao ni kati ya 7-9 gm/ml, upungufu wa damu mkali (severe anaemia) ambao ni kati ya 4-7 gm/ml na upungufu wa damu mkali zaidi (very severe anaemia) ambao ni chini ya 4gm/ml.
Mzunguko wa madini ya chuma mwilini
Kwa kawaida mwili wa mwanamke huifadhi gramu 3.5 mpaka 4.5 za madini ya chuma. Asilimia 75 huifadhiwa kama hemoglobin katika chembe damu nyekundu, asilimia 20 kama ferritin katika mifupa na asilimia 5 inayobaki huifadhiwa katika misuli na vimeng’enyo vingine vya mwili.
Wanawake wasio wajawazito hupoteza karibu gramu 1 za madini ya chuma kutoka katika seli za mwili zinazokufa kila siku na gramu 1 zaidi kila siku wanayokuwa kwenye hedhi.
Ukubwa wa tatizo
Upungufu wa damu kipindi cha ujauzito ni tatizo linalowakumba kina mama wajawazito wengi sana, siyo tu Tanzania bali nchi nyingi zinazoendelea. Inakisiwa kuwa karibu theluthi moja ya wajawazito katika miezi mitatu ya mwisho ya ujauzito hukumbwa na tatizo hili.
Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), inakadiriwa kuwa karibu asilimia 4-16 ya vifo vinavyotokana na ujauzito husababi,shwa na upungufu wa damu.
Aidha,, upungufu wa damu wakati wa ujauzito huongeza uwezekano wa madhara kwa mtoto ikiwemo kifo.
Chanzo cha upungufu wa damu wakati wa ujauzito
Kipindi cha ujauzito huambatana na mabadiliko mbalimbali ya mwili.

0 comments:

Post a Comment