Wednesday 20 August 2014

PUMU YA NGOZI (ECZEMA)



Pumu ya ngozi au kwa kitaalamu Eczema (atopic dermatitis au atopic eczema) ni maradhi ya ngozi ambayo yamefanyiwa utafiti muda mrefu sana na kusema ukweli andiko langu hili halitoweza hata kuandika robo ya yale yanayofahamika kitaalamu kuhusiana na pumu ya ngozi.

Maradhi haya kwa kifupi yamekuwa yakiathiri watoto wengi ulimwenguni na yamekuwa yakisumbua akili za wanasayansi na watabibu kote ulimwengu kwa muda mrefu.

Neno Eczema ambalo ndio jina la maradhi haya kwa kitaalamu ni neno la Kigiriki na linamaanisha kututumka sehemu ya nje ya ngozi, hali ambayo huonekana pale mtoto anapopata maradhi haya.

Maradhi haya ya ngozi yanachangia asilimia arobaini (40) ya maradhi yote ya ngozi yanayoripotiwa hospitalini.

Shambulizi lake

Maradhi haya hushambulia zaidi watoto na huweza kupitiliza mpaka ukubwani, pia lakini kwa wengi huwa yanapungua kadri mtoto anavyokua. Watafiti mbalimbali wanasema kuwa kumekuwa na ongezeko la maradhi haya katika kipindi cha miaka ya usoni hali inayoashiria kuwa maradhi haya ni ya kurithi (atopic eczema)

Karibu asilimia themanini (80) ya wagonjwa wa pumu ya ngozi huanza kuugua maradhi haya wakiwa chini ya umri wa miaka mitano (5). Wagonjwa wengi pia huonyesha dalili za maradhi haya wakiwa na umri chini ya mwaka mmoja.

Maradhi haya pia huweza kujitokeza ukubwani ingawa ni mara chache sana hali hii huonekana.

Maradhi haya huathiri watu wa jinsia zote kwa uwiano sawia yaani wanaume na wanawake.

Dalili zake

Maradhi haya ni ya muda mrefu nikimaanisha kuwa mtu huweza kukaa nayo kwa muda mrefu, ingawa si kuwa muda wote ngozi huonyesha dalili za maradhi. Watu wenye maradhi hupitia vipindi ambavyo ngozi hututumka na kuonyesha dalili za maradhi na vipindi ambavyo ngozi huonekana kama imepona ovyo kutoonyesha dalili yoyote ya maradhi.

Dalili za pumu ya ngozi ni kama zifuatazo:

-Sehemu ya ngozi iliyoathirika huwa inakuwa kavu (inaonekana kavu),

-Sehemu ya ngozi iliyoathirika huwa inatutumuka,

-Ngozi huwasha na kama ukikuna kwa muda mrefu basi hupasuka na kuweza kusababisha vidonda.

-Eneo la ngozi lililoathirika mara nyingine huuma.

-Ngozi huwa inakua na mipasuko inayoweza kuruhusu vimelea vya maradhi kushambulia sehemu za ndani za ngozi.

-Muwasho wa ngozi huwa mkali zaidi nyakati za usiku

-Maeneo yenye athari huwa yanavimba (au kututumka) na kuwa na joto.

-Maeneo ya ngozi yaliyoathirika huweza pia kuwa na malengelenge na hata kutoa majimaji.

Dalili za pumu ya ngozi ni kama zifuatazo:

-Zaidi ya eneo la ngozi kututumka vivimbe pia huweza kuonekana kwenye maeneo ya ngozi yaliyoathirika.

-Bila matibabu ya haraka ngozi inaweza fanya vidonda.

Ingawa maeneo yenye athari huweza kutokea sehemu yoyote ya mwili lakini pumu ya ngozi hupenda kushambulia sehemu zifuatazo

-Mikono hususan eneo baada ya kiwiko kwenda chini

-Miguu

-Viganja vya mikono

-Eneo la nyuma ya magoti (mkunjo wa mguu kwenye eneo la goti)

-Maungio ya mkono kwenye kiwiko

-Shingo

-Sehemu ya juu ya kifua

-Wagonjwa wengine hupata mashambulizi kwenye maeneo yanayozunguka macho na kama mgonjwa atafikisha macho basi maradhi husababisha madhara kwenye macho kutokana na hali ya mgonjwa kukuna macho yake kwa muda mrefu.

-Watoto wengi hupata pumu ya ngozi kwenye uso.

Kujitutumua kwa ngozi huweza kuonekana kwa muda wa siku chache mpaka miezi.

Wagonjwa wa pumu ya ngozi hutofautiana na kwa wengine hupata maradhi sehemu chache tu za mwili wakati wengine hupata sehemu kubwa zaidi za mwili.

Kwa wenye pumu ya ngozi mbaya kabisa sehemu kubwa zaidi ya mwili hututumka na vidonda hutokea pamoja na kutokwa na majimaji kwenye maeneo yenye vidonda.

Bahati mbaya kuhusu maradhi haya ni kuwa eneo la ngozi linapoanza kuonyesha dalili za maradhi haya huanza na umwasho ambao husababisha mgonjwa kujikuna hali ambayo husababisha mikwaruzo kwenye ngozi ambayo nayo husababisha vimelea vya maradhi kuweza kupenya na kusababisha vidonda vikubwa zaidi kutokea kwenye eneo hilo la ngozi. Vidonda vinapotokea husababisha mgonjwa kupata msongo ambao husababisha madhara mengine ya kisaikolojia hasa kama maradhi haya yametokea kwa mtoto mdogo.

Kama hali hii ikitokea kwa mtoto aliye shule basi hata mahudhurio yake shuleni huwa mabaya na hata uwezo wake darasani hupungua.

Sababu za mashambulizi zaidi

-Kuogea maji ya moto kwa muda mrefu

-Kuruhusu ngozi ya mwili kukaa ikiwa kavu kwa muda mrefu (bila kupaka mafuta)

-Kuwa na msongo wa mawazo

-Kubadili joto la mwili (kusafiri kutoka kwenye eneo lenye joto kwenda lenye baridi au kinyume chake)

-Kuvaa mavazi yasiyo ya pamba (cotton)

-Uvutaji wa sigara

-Kukaa kwenye vumbi

-Kukaa kwenye mchanga

-Matumizi ya mafuta ya mwili yanayosababisha mzio wa mwili

-Matumizi ya sabuni zinazosababisha mzio wa mwili

-Ulaji wa chakula kinachosababisha mzio wa mwili (mfano, wale wenye mzio wa vyakula vinavyopatikana kwenye maji/bahari)

Sababu za pumu ngozi

Wanasayansi wanasema kuwa mtu mwenye maradhi haya huzaliwa nayo na kuwa huwa yanarithiwa. Athari za maradhi haya huzidi kutokana na sababu nyingine za ndani au nje ya mwili.

Vitu kama manyoya ya wanyama au mbegu za mimea huweza kusababisha mzio ambao huweza kusababisha madhara makubwa zaidi kutokea kwenye ngozi.

4 comments:

  1. kuna mdogo wangu anazo dalili za hyo pumu ngozi matibabu yake ni yapi

    ReplyDelete
  2. makala ni nzuri lakini imeishia hewani

    ReplyDelete
  3. Nitafute nipate kumtibu maradhi yake.Unaweza kunitafuta kwa Mawasiliano Maalim Saad Email barua ya pepe. fewgoodman@hotmail.com What's App +905344508169

    ReplyDelete