Friday 6 March 2015

WARTS UGONJWA UNAOATHIRI SEHEMU ZA NYETI ZA WANAUME NA WANAWAKE



Warts inaweza kutokea kwenye mikono. Sehemu zilizoota vinundu ni vinyama vilivyoota na ukiviangalia kwa makini vinamwonekano kama taulo.

Ni ugonjwa ambao pia unaweza ukatokea kwenye kiungo chochote cha mwili kama vile usoni na mikononi.


Zinaa ni miongoni mwa magonjwa ambayo yanaongezeka kila siku na sababu kubwa ni jamii kutokuwa na utaratibu wa kupima afya mapema na hivyo kuchelewa kupata matibabu sahihi. Matokeo yake ni kusababisha madhara makubwa.


Warts ni miongoni mwa magonjwa hayo. Watu wengi waliopatwa na ugonjwa huo hawaonyeshi dalili zozote.


Daktari bingwa wa Magonjwa ya Uzazi na Ngozi wa Kituo cha Magonjwa ya Maambukizi (IDC), Dk Goodluck Mushi anasema ugonjwa wa Warts unaoambukizwa kwa njia ya kujamiiana.


Dk Mushi anasema Warts kwa jina jingine ni nyama zinazotokea sehemu za siri katika uume au uke au ndani ya uke pia katika haja kubwa sehemu ya pembeni au katika mashavu ya ukeni.


Ugonjwa wa Sunzua ama warts husababishwa na virusi aina ya Human Papilloma (HPV), ambavyo husambaa kutoka kwa mtu mmoja mpaka mwingine kwa njia ya kujamiiana kunakohusisha njia ya haja kubwa, uke au ngono ya mdomoni.


Anasema mbali na sehemu hizo pia sunzua hutokea pembeni ya mdomo au katika ulimi.


Anasema kati ya watu 100 wenye magonjwa ya zinaa, 40 wana virusi vinasababisha ugonjwa huo wa warts.


Anasema asilimia kubwa ya watu wanaougua ugonjwa huo ni wanawake kutokana na maumbile yao.


Kwa upande wa mwanaume anapata kutokana na michubuko na hivyo virusi hivyo huingia katika njia ya mkojo na mwanaume anaweza kumwambukiza mwanamke kwa kumwagia mbegu.


Hali ikoje mikoani?


Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Watoto kutoka Hospitali ya Wilaya ya Bariadi, Dk Nicholas Mbasa anasema kati ya wanawake 200 ambao walifika katika hospitali hiyo kutibiwa asilimia 38 waligundulika kuwa na ugonjwa wa Warts katika kipindi cha mwaka 2013 pekee.


Dk Mbasa ambaye pia ni specialist wa Magonjwa ya kifua kikuu na ukoma anasema tatizo la ugonjwa huo linaongezeka kila siku kutokana na uelewa mdogo kwa baadhi ya jamii.


Anasema baadhi ya wanaume walio katika ndoa ambao huomba kufanyiwa tohara katika hospitali hiyo, wengi wao wanakutwa na ugonjwa huo na kuanzishiwa matibabu.


Mikakati kuukabili


Dk Mbasa anasema moja kati ya mikakati inayoendelea kwa nchi nzima ni katika kupambana na ugonjwa huo ni kutoa elimu na kuhamasisha jamii kwenda katika vituo vya kutolea tiba kwa ajili ya uchunguzi na tiba sahihi.


“Vilevile tunaendesha kampeni za tohara kwa wanaume kwani wanaume wanaotahiriwa hupunguza uwezekano wakupata warts kwa asilimia 77 hadi 95, huku upande wa maambukizi ya VVU, mwanamume ambaye amefanyiwa tohara hupunguza uwezekano wa kupata VVU kwa asilimia 60,” anasema.


Kundi hatarini


Daktari bingwa wa magonjwa ya kuambukiza na yasiyoambukiza kutoka Kliniki ya MediCorps, Francis Makwabe anasema watu walio na umri kuanzia miaka 14 hadi 35 wapo katika hatari ya kupata ungojwa huo hususan wanawake waliovunja ungo na wale walikatika umri wa kuzaa.


Dk Makwabe anasema wenye mimba wapo katika hatari ya kupata sunzua kwa sababu mama mjamzito anakuwa na upungufu wa kinga ya mwili.


Vilevile, anasema wagonjwa wa kisukari wapo katika hatari ya kupata ugonjwa huo kutokana na kupungua kwa kinga ya mwili pamoja watu wanaotumia dawa kali. Kundi jingine lililopo katika hatari ya kupata warts, analitaja ni la wale wanaofanya mapenzi kwa njia ya mdomo, kuwa na mpenzi zaidi ya mmoja na kufanya ngono kinyume cha maumbile.


Mbali na kundi hilo vilevile watoto wadogo wanaweza kuambukizwa ugonjwa huo kwa kufanyiwa vitendo vya ubakaji.


Dalili zake:


Moja kati ya dalili za ugonjwa huo ni kuwa na vinyama au vinyuzi nyuzi mithili ya taulo laini katika sehemu za siri ambapo mara nyingi huwasha wakati wa joto au unaponyoa nywele sehemu za siri.


Vinaweza kuota pia kwenye ulimi, mashavu ya uke, mapajani, katika lips za mdomo na usoni.


Vinyama hivyo pia vinaweza kutokea usoni, hasa sehemu karibu na kope ama maeneo mengine kama vile vidole vya miguu na mikono.


Madhara


Warts inaweza kubainika kwa vipimo vya maabara. Warts zikitokea katika shingo ya kizazi, inaelezwa kuwa inasababisha saratani ya kizazi kwa wanawake na kwa upande wa wanaume inasababisha kansa kwenye sehemu ya njia ya mkojo.


Anasema mtu wenye maambukizi ya virusi vya Ukimwi yupo katika hatari ya kupata ugonjwa huo kwa sababu nyama hizo huota na kukua kwa haraka kutokana na upungufu wa kinga iliyoshuka.

Matibabu


Dk Mushi anasema licha ya ugonjwa huo kusababisha madhara kwa binadamu, ikiwamo saratani na kukosa mtoto, lakini unatibika ikiwa mgonjwa atawahi matibabu.

4 comments:

  1. Nimejifunza mengi sana dokta barikiwa kwa kazi yako!

    ReplyDelete
  2. Mwenyenzi akuzidishie"pamoja niko dar

    ReplyDelete
    Replies
    1. Kwa Sote Ndugu HD Mavoice Ubarikiwe na wewe.

      Delete