Tuesday 23 September 2014

WHO YATOA TAHADHARI KWA WANAOTUMIA SUKARI NYINGI




 


WATAALAMU wa afya wametahadharisha kwamba juhudi zaidi zinahitajika kufanyika kupunguza kiwango cha sukari kinachotumiwa na watu.

Shirika la Afya Duniani (WHO), kushirikiana na washauri wa masuala ya afya nchini Uingereza, wamependekeza watu kupunguza viwango vinavyopendekezwa vya kutumia sukari mwilini.

Kwa mujibu wa BBC, ushauri mpya unasema kwamba, kiwango kinachostahili cha sukari mwilini ni asilimia tano kutoka asilimia 10.

Hata hivyo, utafiti mbadala unasema kwamba kiwango kinachofaa hakipaswi kuwa zaidi ya asilimia tatu.

Watafiti wamesema kwamba ushauri huo mpya unahitajika kuzingatiwa, ikitiliwa maanani gharama ya matibabu kwa sekta ya afya, hasa matibabu ya magonjwa ya meno.

Wametahadharisha zaidi kwamba sukari ni kiungo muhimu katika kuchochea magonjwa ya meno, ambayo, hata hivyo, yanaweza kuzuilika.

Utafiti unaonyesha kuwa kutumia kiwango kikubwa cha sukari mwilini kunaongeza uwezekano wa meno kuoza na kuharibika hususan kwa watoto.

Matibabu ya magonjwa ya meno hugharimu nchi zilizostawi kati ya asilimia tano na 10 ya matumizi ya pesa za matibabu.

Wataalamu hao wameitaka serikali ya nchi hiyo kudhibiti upatikanaji wa mashine za kuuza soda na vinywaji vingine vyenye sukari na hata kuziondoa katika maeneo ya shule na hospitali.

0 comments:

Post a Comment