Thursday 29 May 2014

KUWA NA KIUNGULIA KILA MARA KUNAWEZA KUSABABISHA KUPATWA NA KANSA YA KOO KWA ASILIMIA 78%


Kiungulia ni hali inayojitokeza kwa mtu kuhisi maumivu ya kuwaka moto yakianzia maeneo ya chini ya kifua yakipanda katikati ya kifua hadi kufikia katika usawa wa kooni.
Hali hii ya kuhisi kuwaka moto kooni au kifuani husababishwa na tindikali au acid iliyoko tumboni ambapo tindikali hii inakuwa inapanda juu kutoka tumboni kutokana na matatizo mbalimbali katika mfumo wa tumbo na miongoni mwa matatizo ni mtu kuwa na tatizo la kuzalishwa tindikali nyingi zaidi tumboni kuliko mahitaji halisi.
Mpenzi msomaji, kutokana na tafiti zilizofanywa, imegundulika kuwa, mtu kuwa na kiungulia cha mara kwa mara huwa hatarini kupata tatizo la kansa ya koo kwa asilimia 78, na hii ni kwa watu ambao siyo watumiaji wa pombe na pia kwa wasiotumia au kuvuta sigara.
Tafiti hizo zilizofanyika nchini marekani na kuchapishwa katika jarida maalumu la habari za kitafiti za magonjwa ya kansa, A journal of the American Association for Cancer Research, pia zimeeleza kuwa, dawa zinazotumika kupunguza tindikali (Antacids) zimeonekana kusaidia kupunguza hatari ya mtu kupata kansa ya koo inayosababishwa na kiungulia cha mara kwa mara, lakini kwa dawa zinazotumika kuua vijidudu vinavyosababisha magonjwa, antibiotics, hazina msaada katika kupunguza hatari hii ya kansa ya koo.
Mpenzi msomaji, katika tafiti hiyo utaona kwamba, inawezekana mtu tatizo la kuwa na kiungulia akaliona ni kitu kidogo sana, na hata akaacha kuchukua hatua zinazostahili ili kuondokana na hali hiyo, lakini mwisho wake ni kuja kupata tatizo kubwa zaidi, kansa, utahitaji muda mwingi zaidi, gharama kubwa na kupitia matibabu magumu ili kuithibiti kansa ya koo.
Sasa ni wakati wa kubadilika, tujiepushe na vitu vinavyoweza kuleta kiungulia. Tuwe na utaratibu maalumu wa kula chakula kwa maana ya kutokaa na njaa kwa muda mrefu ambapo pia itasaidia kuepuka vidonda vya tumbo, kukiandaa chakula vizuri kabla ya kukipika mfano maharagwe ambayo huwa na tindikali asilia nyingi, ulaji wa matunda mfano mapapai au ndizi, kunywa maji ya kutosha hata kama hauna kiu na pia kufuata ushauri wa wataalamu wa afya kulingana na hali yako ili kuweza kuishi katika afya nzuri zaidi.

0 comments:

Post a Comment