Saturday 3 May 2014

MENOPAUSE: USIHOFU, NI UTU UZIMA WA MWANAMKE NA MABADILIKO YAKE -2

 
 
Kwa bahati mbaya dhana hii potofu bado ipo miongoni mwetu. yamejengeka mawazo kuwa menopause ni kipindi kigumu kinachoweza kumfanya mama awe kichaa, na hata kufikia hatua ya  kumdunda mwenza wake!
 
Kwa kuwa mabadiliko yanayosababisha hali hii ni mengi na mapana, nitajadili mabadiliko yanayoletwa na hali hii na jinsi ya kuyakabili.
 
Kwa akina mama mama wengi, hedhi inaanza katika umri wa takribani miaka 14 na kukoma katika umri nilioutaja mwanzo. Katika hali ya kawaida, kuona au kutoona hedhi 
 
kunasababishwa na kuwepo au kutokuwepo kwa mzunguko wenye uwiano mzuri wa homoni nne kuu; mbili zikiwa 
 
zinatengenezwa na tezi za kutengeza mayai ya uzazi na ambazo ni kuu katika maisha ya uzazi wa mwanamke: estrojeni na projesteroni na zingine mbili toka kwenye 
 
ubongo.
 
Homoni hizi ndizo zinasababisha kukua na hatimaye aghalabu yai moja kupevuka na kutoka katika tezi moja kati ya mbili alizonazo mama kila mwezi.  Kama yai hili 
 
litakutana na mbegu ya kiume, basi mama atatunga mimba na tangu hapo hedhi inakoma mpaka baada ya kujifungua.
Kama itakuwa vinginevyo, utando wa ndani ya mfuko wa 
 
uzazi wa mama ambao ulikuwa umeandaliwa na mabadiliko ndani ya mwili wa mama kuitunza mimba kwa sababu ya homoni hizi, unatoa damu tunayoiita hedhi. Mara nyingi mzunguko huu unajirudia kila mwezi mpaka mama 
 
anapofikia menopause.
Ikitokea kuwa mfumo wa kutengeneza homoni hizi au uwiano wake katika mwili una shida au vyote viwili, hedhi 
 
ya mama inakuja kwa mpangilio usio mzuri. Aghalabu hili ni jambo la kawaida katika miaka ya mwanzo ya hedhi (miaka minne hadi sita ya mwanzo wa hedhi) na miaka miwili hadi 
 
minane kabla ya menopause.
 
Matatizo yanayotokea mama anapokaribia menopause yanasababishwa na mambo makuu manne. Mosi, ni ukweli kwamba homoni mbili muhimu katika mpangilio wa kuona 
 
hedhi kila mwezi kwa mpangilio zinaanza kutengnezwa katika mfumo usiotabirika sana na tezi za mama.
 
Hali hii inasababisha hedhi kutotabirika; yaweza kuja mara kwa mara au baada ya muda mrefu na kwa baadhi ya akina mama inaambatana na damu nyingi isiyo kawaida yao.
 
 Pili, ni mabadiliko yanayoambatana na vichomi joto (hot flushes) kichwani, shingoni na kifuani ambavyo aghalabu huambatana na hisia ya joto jingi mwilini na kutoka jasho 
 
jingi hasa wakati wa usiku. Kwa kawaida hali hii inachukua sekunde au dakika chache ingawa kwa nadra yaweza kuchukua saa moja hivi na inatokea na kujirudia mara kwa 
 
mara.
Hali hii inaweza kuleta usumbufu mkubwa na hali ya wasiwasi katika maisha ya kila siku ya mama.
 
 
Tatu, ambalo nalo linasababishwa na upungufu wa homoni nilizozitaja ni baadhi ya viungo vya mama kuanza 
 
kuonyesha hali ya uzee kama vile viungo kulegea kinyume na hapo mwanzo. Mabadiliko haya hutokea katika viungo mbalimbali vikiwemo vya uzazi. Ni wakati huu ambapo ngozi 
ya mama inaanza kulegea, mama kuwashwa sehemu za siri na kupata matatizo mbalimbali katika mfumo wa mkojo kama vile kusikia maumivu anapokojoa na baadhi hata kushindwa kuuzuia mkojo wanapopata hisia za kukojoa.
 
Mwisho ni matatizo ya kiafya yanayoweza kutokea miaka mingi baada ya hedhi kukoma kwa sababu ya ukosefu wa homoni ya oestrogeni kama mifupa ya mama kupoteza uimara wake na magonjwa yanayohusiana na mzunguko wa damu na moyo.
 
Ingawa mwanzoni kulikuwa na dhana kuwa akina mama wengi wa Kiafrika hawapati matatizo mengi yanayohusiana na mifupa kupoteza uimara baada ya kufikia menopause, ushahidi wa karibuni unaonyesha kuwa yawezekana magonjwa haya si nadra kama ilivyofikiriwa.
 
Pengine sababu kubwa iliyojenga dhana hii ni kukosekana kwa akina mama wengi wa Kiafrika wanaoishi kufikia umri wa miongo saba au zaidi. Ni wakati huu ambao akina mama 
 
wanaweza kuvunjika mifupa kirahisi na kama huduma za matibabu sio nzuri, hali hii inaweza kusababisha vifo.
Ikumbukwe kuwa mifupa ya mama inajengeka kwa kasi 
 
mara baada ya kuvunja ungo na mara nyingi kasi hii inakoma kabla ya kufikia umri wa miaka thelathini. Baada ya umri huu, taratibu mifupa ya mama inaanza kuwa dhaifu 
 
na hali inaendelea kwa kasi baada ya kufikia menopause mpaka takribani miaka kumi na tano baada ya hapo.
Chakula chenye madini mengi ya calcium na vitamini D
 
mazoezi ya mwili na kuepuka unywaji pombe wa kupindukia na uvutaji sigara, ni vitu muhimu vinavyosaidia kuifanya mifupa ya mama kuwa imara.
 
Bahati nzuri akina mama wengi wa Kiafrika wana mifupa imara zaidi kuliko akina mama wa nasaba zingine, na hivyo kuishi maisha yanayosaidia kuifanya mifupa imara zaidi 
 
kunaweza kuchelewesha madhara mengi yanayotokana na matatizo ya mifupa yanayotokana na utu uzima.
Vile vile ikumbukwe kuwa katika hali ya maisha 
 
yanayozingatia afya njema, magonjwa ya moyo na presha  si mengi miongoni mwa akina mama walio katika umri wa 
 
kupata hedhi kama ilivyo kwa wanaume wa umri sawa, lakini hali hii inabadilika baada ya menopause ambapo jinsia zote zinakuwa katika uwezekano sawa wa kuugua magonjwa haya.
 
Kwa bahati mbaya umri wa menopause na baada ya hapo ni wakati ambao binadamu wengi wanakumbana na matatizo mbalimbali ya kimaisha na kiafya bila kujali jinsia na wale 
 
wanaoishi miaka mingi zaidi kama akina mama.
Kwao, hiki ni kipindi cha kuwapoteza wenzi wao, kukosa huduma mbalimbali za kiafya hasa katika jamii zisizo na 
 
mfumo imara wa huduma za afya, na pia ni kipindi cha kustaafu kutoka katika ajira zao au kupungukiwa na nguvu 
 
za kufanya shughuli za awali za kuwaingizia kipato cha uhakika, na hivyo kulazimika kuishi maisha mapya na 
 
pengine magumu kuliko awali. Ikitokea mama akapata matatizo ya kiakili wakati huu, ni rahisi sana kuyahusisha na hali ya mabadiliko yake.
 
Vilevile ikumbukwe kuwa magonjwa ya mfadhaiko (depression) mara nyingi yanawapata wanawake kuliko wanaume, na yakitokea wakati huu si ajabu yakahusishwa 
 
na mabadiliko yanayompata mama!
Maisha ya mama wakati huu yanategemea, kwa kiasi kukubwa, jamii iliyomzunguka na matarajio ya jamii hiyo 
 
kwake.  Kama jamii husika ina misingi fulani ya maisha, basi, mama ataifuata. Kwa mfano, kama si kawaida mama kumdunda mume, ni nadra mama kufanya hivyo kwa sababu 
 
tu amefikia menopause kwa sababau suluhu ya matatizo ya ndani ya nyumba yatatatuliwa kwa njia na utaratibu wa 
 
jamii husika.
Ni nini cha kufanya katika umri huu? Vi vyema jamii, mama na wahudumu wa afya waelewe mabadiliko haya na kumsaidia mama kama inavyostahili. Jamii ielewe kuwa 
 
watu wengi kwa baraka za Mungu na huduma nzuri za afya wanaweza kuufikia umri huu na kwamba mabadiliko yanayotokea ni ya kawaida katika maisha ya binadamu.
 
Zamani katika jamii nyingi za Kiafrika, huu ulikuwa ni wakati ambao mama alikuwa na wajukuu, na hivyo kuitwa nyanya na aliweza kupewa majukumu yaliyo wazi na mara 
 
nyingi alisaidiwa katika shughuli mbalimbali. Bahati mbaya ukaribu huu umeanza kufutika kwa sababu ya mfumo wa 
 
maisha ya sasa.
Hata hivyo, wahudumu wa afya katika ngazi zote hawana budi kuelewa hali hii na pale inapowezekana mama aambiwe mabadiliko yanayotokea mwilini mwake na pengine  
 
kumsaidia amwone daktari bingwa wa magonjwa ya akina mama aliye karibu kwa ushauri na tiba kama inahitajika.
Bahati nzuri matatizo mengi niliyoyataja yanaweza kutibika au kupunguzwa makali yake.
 
 Nasisitiza kuwa ni vyema wahudumu wa afya wawe na ujasiri wa kuwauliza akina mama hawa mambo mbalimbali yanayohusiana na mabadiliko yanayowapata na siyo kusubiri mama aeleze kama anayapata au la.
 
Yumkini matatizo yanaweza kuwepo lakini mama akaona aibu akuyasema au kufikiri ndio uzee wenyewe na kuamua kufa ‘kisabuni’. Kwa mfano, wengi wa mama hawa wanaendela na maisha ya unyumba na pale yanapotokea 
 
matatizo, hakuna budi wasaidiwe kuweza kufurahia maisha haya kama watu wengine.
 
Akina mama hawa ni mama, nyanya, dada, shemeji na hata jirani zetu, na zaidi ya yote ni Watanzania na binadamu wenzetu. Hakika, wanahitaji msaada wetu sote.

0 comments:

Post a Comment