Saturday 27 September 2014

NJIA YA KUPUNGUZA MAUMIVU WAKATI WA KUJIFUNGUWA MTOTO-3



Mpenzi msomaji, leo namaliza makala haya niliyoyaanza wiki tatu zilizopita. Ungana nami ili upate darasa kuhusu njia ya kupunguza maumivu wakati wa kujifungua...
Katika Jarida la American Baby, mtaalamu mmoja aliwahi kuandika faida ya mwanamke mjamzito kufanya mazoezi wakati wa ujauzito yenye lengo la kumuwezesha kuwa na pumzi ya kutosha. Wengi kati ya wanawake hupenda zaidi kula na kuwa wavivu kufanya kazi au mazoezi, jambo ambalo huongeza uzito wa mwili na kuathiri mfumo wa upumuaji.
Haishauriwi mjamzito kushinda amelala au kukaa, ni vema akamuona daktari amshauri kuhusu aina ya mazoezi kulingana na umri wa ujauzito wake. (Onyo mwanamke asifanye mazoezi bila ushauri.)
Lakini pia muuguzi Ina May Gaskin, anasema katika maneno yake kwamba kuamini kwamba ujauzito si tatizo ni njia ya kuujengea mwili uwezo wa kukabiliana na maumivu wakati wa kujifungua.
Labda swali ni kwamba wanawake wangapi wanaosaidiwa kujiamini wakati wa ujauzito wao? Kipimo cha tatizo hili kinaweza kuwa ni kigumu lakini ikiwa mjamzito anaishi kwa hofu nyingi zitokanazo na matatizo ya kujifungua ni dhahiri hajiamini.
Njia nyingine ya kupunguza maumivu wakati wa kujifungua inatajwa kuwa ni kupenda mtoto atakayezaliwa. Mapenzi haya ya kupata mtoto yanaweza kumsaidia mama mjamzito akavumilia na kuyaona maumivu kuwa si kitu zaidi ya kujifungua. Ushahidi wa hili unapatikana kwa wanawake wanaoamua kutoa mimba baada ya kutopenda kuzaa. Kwao maumivu huwa ni kitu kidogo ukilinganisha na nia yao ya kutoa mimba.
Aidha, nilidokeza hapo juu umuhimu wa kufanya mazoezi, lakini ukweli ulio wazi umebainika kuwa wanawake wanaotembea tembea wodini au nje kipindi cha kuelekea kujifungua hupata nafuu ya maumivu, kuliko wanaoketi na kulia.
Utafiti uliofanywa hivi karibuni na timu ya wataalam nchini Marekani ulionyesha wanawake waliotazama picha za wapenzi wao wakati wanaugulia maumivu ya uzazi walitabasamu na kutulia, huku picha za watu waliowachukia zikitajwa kuwaongezea hangaiko.
Jambo kubwa la kukumbuka ni kwamba maumivu na presha ni vitu vinavyokwenda sambamba, hivyo haishauriwi kwa mtu mwenye maumivu kuwa na fikra mbaya, wasiwasi au kuogopeshwa.
Nimalizie tu kushauri kwamba mjamzito anatakiwa kuwa karibu na wataalam wa saikolojia ili kupata msaada wa kukabiliana na hofu ya uzazi ambayo ni hatari zaidi kwa uzazi salama.
Ushauri wa mwisho kama mwanamke anataka kupunguza maumivu wakati wa kujifungua awe hodari kuhudhuria kliniki na aweze kuuliza kila jambo analohisi linamtatiza.
Lakini pia ni mwiko wa kitabibu kwa wakunga kuwatia hofu wajawazito kwa kuwaambia maneno ya kukatisha tamaa. Hata kama tatizo lipo mjamzito atiwe moyo kwa kuambiwa; “Mtoto amekaa vibaya, lakini ukifanya hivi na vile utajifungua salama tu.”

0 comments:

Post a Comment