Saturday 27 September 2014

NAMNA YA KUISHUGHULIKIA NA KUISHINDA HOFU






Hofu na mashaka ndiyo adui namba moja anayefilisi nguvu au nishati ya mwili wa mwanadamu kwa haraka kuliko kitu kingine chochote. Wengi wameathiriwa katika maisha yao ya kielimu, kiafya, kijamii, kikazi na hata kiuchumi kwa sababu ya hofu au mashaka.

Wengi wameshindwa kufikia malengo na ndoto zao katika maisha kwa sababu ya hofu na mashaka.

Mara tu hofu na mashaka vinapoingia ndani ya mtu hudumu kwa muda mrefu huku vikileta uharibifu mkubwa katika nafasi, akili, na maendeleo ya mtu huyo kwa ujumla. Makala au mada hii itakuwezesha kufahamu kwa kiasi kikubwa mambo unayoweza kufanya ili kuondokana au kupunguza athari za hofu na mashaka na pia kuweza kutoa msaada kwa yeyote anayepitia tatizo hili kwa wakati fulani.

Hofu ni mjumuiko wa kujali kusiko na sababu yoyote (unnecessary concern) au kusiko na maana yoyote juu ya nafsi au utu wa mtu. Tunasema hakuna sababu wala umuhimu wowote kwa sababu kujali huku kumejengwa katika misingi ifuatayo;

Mtu kujali sana au kuweka mawazo sana katika vitu ambavyo viko nje ya uwezo wake.
Mtu kuanza kusikitikia mambo yajayo badala ya kujipanga na kujiandaa kuyakabili pale yatakapowadia.
Kuweka msisitizo zaidi katika jambo moja na kuyasahau mengine. Anayehofu hudhani kwamba ikiwa kile anachokiwekea msisitizo kitashindikana, basi kila kitu kitakuwa kimeharibika.

Mtu kushindwa kutumainia imani aliyonayo juu ya ufanisi wa jambo fulani. Hofu yake katika jambo fulani huizidi imani aliyonayo na kwahivyo hali ya kushindwa kuonekana dhahiri zaidi kuliko hali ya kushinda.

Kwa sababu hofu hujengwa katika fikra zisizo na maana wala uhalisi wowote, basi njia ya kuiweza hofu hiyo ni lazima iwe kwa kutumia fikra zenye maana na uhalisi ili kuushinda uwezo wako wa kufikiri kushindwa.
Yafuatayo yatakusaidia kukuwezesha kupunguza kiwango cha hofu katika maisha.

Jiulize swali “Je, nini kinachoniangamiza?”
Hofu ni kitu kinacho angamiza, tena huangamiza kwa viwango na hatua tofauti. Ngoja nijaribu kukupa mfano wa maelezo.

Hofu kwa lugha ya Kingereza ni “worry” neno “worry” limetokana na lugha ya Kidachi lenye maana ya “Worgen”. Maana ya neno “worgen” ukiipeleka moja kwa moja katika lugha ya Kiingereza humaanisha “strangle”. Maana ya neno “strangle” kwa lugha ya Kiswahili ni “Kunyonga kwa kamba”. Sasa yamkini hapa unanielewa kwanini ninasema hofu huua au kuangamiza.

Uzuri ni kwamba, hofu haiangamizi pasipo kutoa tahadhari kabla, baadhi ya tahadhari zinazotolewa katika mchakato wa kuangamizwa na hofu ni pamoja na hamaki za mara kwa mara, mvi za mapema, baadhi au upele fulani wa ngozi, vidonda vya tumbo (ulcers), matatizo ya kukosa usingizi, kuhitaji kwenda haja ndogo mara kwa mara n.k.

Swali hili la “ni nini kinachoniangamiza?” litakuwezesha kujitathmini wewe mwenyewe.


Namna ya kuishughulikia na kuishinda hofu-2



Wiki iliyopita tulianza kutazama namna ya kuishughulikia na kuishinda hofu. Wiki hii tunaendelea na sehemu ya pili ya mada hii.
Endelea...

Katika kulijibu swali hili utaweza kutathmini kwa kujiuliza kuwa “Ni nini katika maisha yangu ambacho nimekipa kipaumbele zaidi kuliko afya yangu na Maisha yangu? Maana ya swali hili ni ukweli kwamba kama una hofu katika jambo fulani maana yake hilo jambo au hicho kitu umekipa umuhimu au uzito usiostahili kuliko maisha yako. 

Je ni jambo gani au kitu gani umekipa umuhimu au uzito usiostahili katika maisha yako? Je ni kazi yako?, Je ni elimu yako? Je ni ujenzi wa nyumba? Je ni kibali kwa watu? Je ni watoto wako au mwenza wako? Je ni malipo ya mkopo uliouchukua? Kumbuka haitakusaidia wala kukuongezea chochote kwa kujiua ukikiwaza hicho kitu, mwisho mwenye hasara ni wewe.

Hata mwisho kama hautapoteza maisha yako lakini ukadhoofisha afya yako, faida yake ni nini? Na afya yako ikipotea, nini tena utakifanya kuyanufaisha maisha yako?

Kama hofu yako ni kwenye kupata kibali machoni pa watu wanaokuzunguka, labda ofisini, chuoni, mtaani nk. Kumbuka kuwa watu hao wala hawatajali au kukukumbuka pale utakapokuwa unaugulia wodini au nyumbani kwako kisa ni magonjwa yanayohusiana na hofu.
Labda mfano huu waweza kukusaidia zaidi kuelewa ninachomaanisha. 

Kijana mmoja alimuuliza swali mwanafalsafa (philosopher) mmoja akisema, “Nini kinachokushangaza sana kwa huyu kiumbe binadamu?”

Mwanafalsafa alijibu “Ninamshangaa sana kiumbe mwanadamu kwa sababu hupoteza afya yake kwa kiasi kikubwa sana akitafuta pesa, na baadaye hutumia pesa yake yote akiitibu au kujaribu kuirejesha afya yake iliyopotea katika hofu za maisha.

Kwa kuihofia kesho yake, mwanadamu huyu ametumia muda wote wa sasa akijiandaa na hiyo kesho, na matokeo yake, kwa kuichosha sana afya yake ameshindwa kuifurahia leo yake na hata hiyo kesho yenyewe huiona kwa taabu sana” (Mwenye ufahamu na afahamu).

Acha kuyapa mawazo yako au mitazamo yako umuhimu usiostahili.
Hofu, woga na hamaki za mara kwa mara ni alama kwamba unayapa mawazo, fikira na mitazamo yako umuhimu usiostahili. Maana yake ni kwamba kila unaloliwaza au kulifikiri unalichukulia kuwa ni halisi, ingawa mara nyingine ukweli ni kwamba unavyowaza sivyo.

Hakuna ukweli wala uthibitisho kuwa kila unachokiwaza kitatokea.
Hizi twaweza kuziita fikra laini, pale ambapo unadhani kuwa kila unachowaza kitatokea.

Mtu mwenye ukichaa, akiwaza kuwa kuna mtu anataka kumpiga risasi atakimbia huku na huko kujificha. Wakati ukweli ni kwamba hakuna kitu kama hicho. Wewe siyo kichaa, kwa nini uweke vyote unavyoviwaza kama vile ni dhahiri? Tena hususan vile vitu vibaya?

Tabia sugu nyingi walizonazo watu husababishwa na fikra, vile wanavyowaza. Usiruhusu mawazo yako yakufanye mtumwa. 

Mawazo ya kitaalamu yanaonesha kwamba kama ukiweka mawazo yako sana katika kitu fulani, inaweza kuishawishi tabia au utendaji wako katika hali ambayo yaweza kuanza kufanya hofu zako kuanza kuwa kweli. 

Ni kwasababu hii ndiyo maana, unashauriwa kuweka mawazo na fikra zako zote kwenye vitu ambavyo ni vya maana.

0 comments:

Post a Comment