Saturday 3 May 2014

ZIJUE ATHARI ZA DAWA ZA KUULIA WADUDU (VIUATILIFU) KWA AFYA YA BINADAMU NA MIMEA.




VIUATILIFU ni kemikali zinazokusudiwa
kuzuia, kuharibu au kudhibiti visumbufu.
Unapozungumzia visumbufu ni pamoja na
magonjwa yanayoshambulia mimea,
wadudu, magugu, ndege, wanyama, samaki
na minyoo.

Magonjwa haya yanatishia na kusababisha
madhara wakati wa kilimo, uzalishaji,
usindikaji, uhifadhi, usafirishaji au uuzaji wa
chakula, bidhaa za kilimo.
 
Hivyo viuatilifu ni muhimu katika uzalishaji
wa mazao ya kilimo, kwa kuwa viuatilifu
uainishwa kutokana na visumbufu
vilivyolengwa.
 
Mhadhiri Mshauri wa Chuo Kikuu cha
Sayansi na Tiba Muhimbili (MUHAS),
anasema viuatilifu vinaweza kuwa
na madhara kwa binadamu na mazingira
kwa kiwango tofauti na wakati mwingine
vinaweza kusababisha vifo kwa binadamu
na viumbe kila mwaka.

Iwapo vinatumika ni muhimu vikatumika kwa uangalifu kama inavyoshauriwa na wataalamu.
Kila kitu kimetengenezwa na kemikali. Sote
tumetengenezwa na kemikali. Kuna mifumo
mingi ya kikemikali inayoendelea ndani ya
miili yetu.

Mimea ina uwezo wa
kubadili kemikali kama hewa ukaa (kabonidioksaidi), maji na
madini kutoka kwenye udongo kujenga
nyingine za hali ya juu zaidi, kama vile
sukari, protini na mafuta.
 
Mimea na wanyama hutengeneza
na kuvunja kemikali mfululizo ambapo
hutumia kemikali kutuma ujumbe kutoka
sehemu moja kwenda nyingine.
 
“Watu hutumia kemikali nyingi
zilizotengenezwa kiasili, katika karne
iliyopita watu wamekuwa hodari
kutengeneza kemikali.

 
“Tuna sabuni za kuoshea nyumba na
kemikali za kuzuia sabuni hizo zisilipuke au
kuungua,
Kuna kemikali ndani ya vipodozi
vinavyotumika kila siku kama rangi za kucha
na losheni za mikono.
Anasema pia zipo katika bidhaa mbalimbali,
mfano, zebaki (mercury) katika taa za
kuokoa nishati.

Viuatilifu vinaingiaje mwilini?
Inaelezwa kuwa unaweza kula kwa bahati
mbaya au kwa makusudi, vyakula
vilivyokuwa na chembechembe za viuatilifu,
 
kuvuta hewa yenye viuatilifu, kupitia kwenye
ngozi (macho) iwapo utashindwa kutumia
vifaa vya kujikinga wakati wa kuchanganya
na kunyunyizia katika kilimo au hata kupitia
mfuko wa uzazi wa mama mjamzito
kwenda kwa mtoto aliye tumboni.

Pia viuatilifu vinaweza kuingia mwilini
kupitia maji yaliyochafuliwa na kiuatilifu
ambapo si lazima rangi na ladha ya maji
viwe vimebadilika.

Sumu ya viuatilifu
inayoingia mwilini mwa binadamu inaweza
kuwa na athari za papo kwa hapo au athari
za muda mrefu.
 
Dalili za madhara ya viuatilifu katika mwili
wa mwanadamu na mtu
aliyedhurika na viuatilifu huwa na maumivu
ya tumbo, kizunguzungu, maumivu ya
kichwa, kutapika, kukosa hewa, kukohoa,
pamoja na kuwapo kwa matatizo ya ngozi
na macho.

Pia kuna madhara ya muda
mrefu kama vile kupata saratani, msongo
wa mawazo, matatizo ya mfumo wa neva,
 
upungufu wa nguvu za kike na kiume,
mimba kutoka na hata kuwepo kwa
upungufu wa viungo vya watoto
wanaozaliwa.
 
Madhara yanayotokea baada
ya muda mrefu kama kuwa msahaulifu au
kupoteza kumbukumbu, kutetemeka
mikono, kushindwa kuzingatia jambo,
kuonekana mzee kuliko umri halisi, kupooza
na kukosa fahamu.

 
Wanasayansi
wanachunguza sumu za kemikali kwa
kutumia wanyama, kwa kuangalia mifumo
katika mazingira na kuchunguza watu
wanaogusana na kemikali.

“Usumu mara nyingi hutambulika baada ya
majaribio yanayotumia wanyama (panya,
sungura, buku),”

Baada ya majaribio kemikali
hupangwa katika makundi na kuwekewa
kibandiko kutokana na usumu wake.
kuna umuhimu mkubwa wa
kujua alama zinazowekwa katika vibandiko
ili kuweza kujikinga na kujiepusha na athari
zinazoweza kutokea.
 
Makundi yaliyoathirika anayataja kuwa ni
wajawazito, ambapo humuathiri hadi mtoto
aliye tumboni.
Kina mama ambao ni
 
wajawazito hawaruhusiwi kufanya kazi
katika viwanda vinavyozalisha kemikali hizo
kutokana na wakati huo mifumo ya miili yao
kuwa katika mabadiliko.

“Watoto wapo katika kiwango cha juu
kuweza kuathirika kutokana na miili yao ni
midogo na bado inakua,”.

Kundi jingine linaloathirika ni
wazee kwa sababu ya mifumo ya miili yao
kuchoka.

 
Viuatilifu vinaingiaje katika mazingira?
Inakadiriwa asilimia 10 hufikia
lengo lililokusudiwa huku asilimia 90 ya
kemikali hizo zinaishia kwenye mazingira.
Viuatilifu
 
vinapoharibiwa kwa njia zisizo sahihi baada
ya kwisha muda wake vinaweza kuchangia
kuharibu mazingira.
Athari zilizowahi kutokea kutokana na
 
kemikali hizo kuingia katika mazingira ni
pamoja na baadhi ya mayai ya kienyeji
yaliyowahi kuhifadhiwa katika eneo moja
wapo lililokuwa na viuatilifu chakavu kupata
madhara,”

Pia baadhi ya maeneo yaliyohifadhiwa
viuatilifu chakavu hadi sasa mimea haiwezi
kuota tena kutokana na kiwango cha
viuatilifu kuwapo katika mazingira.

Viuatilifu vikitumika kwa
wingi mno huathiri uwezo wa udongo
kushika maji na virutubisho, hudhuru hata
wanyama waishio ardhini na ndani ya maji.

Nashauri kuepuka matumizi
holela ya kemikali na wakulima kutumia
elimu wanayopata kuzingatia wakati wa
umwagiliaji wa kilimo.
 Pia kutumia mbinu mbadala ili
kupunguza matumizi ya viuatilifu.

0 comments:

Post a Comment