Thursday 1 May 2014

VYAKULA AMBAVYO SI VIZURI KULA WAKATI WA KWENDA KULALA KWA WATU WANENE NA WENYE UZITO MKUBWA.




Wengi wanafikiria kuwa unene ni fahari, heshima, lakini huenda wanasahau au hawajui madhara mengi ambayo yamejificha nyuma yake

Imekuwa ikidhaniwa kuwa unene wa mwili ni kufanikiwa kiuchumi au kuukata, kumbe sivyo.  Uchunguzi wa kitaalamu unaonyesha kuwa watu wanene wapo katika hatari ya kupata maradhi ya kiharusi, kisukari na ugonjwa wa moyo.
Matumizi ya baadhi ya vyakula na kutokujua chakula gani wale na kwa wakati gani bado ni tatizo.
Baadhi yao hula vyakula hivyo usiku,  bila kujua athari kuwa vinazidisha unene na kuhatarisha maisha.
Wataalamu wanaeleza kuwa baadhi ya vyakula vikiliwa usiku husababisha athari kwa afya za watumiaji wake.
 
Athari kubwa zaidi ni kuongezeka uzito bila mpangilio, kukosa usingizi na kulala kama mfu kutokana na tumbo kujaa, vilevile kulala kwa usingizi wenye kukatikakatika, kujisaida haja ndogo kila mara. Madaktari na wataalamu wengine wa afya wanashauri kwamba ili kujiepusha na athari hizi ni vyema watu wanene wakatumia matunda, mbogamboga au vyakula vingine ambavyo vina kalori na mafuta kidogo au visiwe navyo kabisa.
Hivi ni baadhi ya vyakula ambavyo si vizuri kula wakati wa kwenda kulala kwa watu wanene na wenye uzito mkubwa.
Vyakula vilivyoandaliwa kwa mafuta mengi
Hii ni aina ya chakula ambacho hupaswi kula usiku kwa sababu havikufanyi ujisikie uchovu na uvivu asubuhi ya siku inayofuata, bali pia humpa msukosuko mtumiaji wa kwenda kujisaidia mara kwa mara.
Pamoja na vyakula vya mafuta, ice cream  ni tatizo kwa kuwa ukila sukari unaongezeka uzito bila sababu, pia hujipa msukosuko wakati wa kulala kwa kuwa baada ya muda huyeyuka na kuzaa tatizo nyingine. Aina hii ya vyakula husababisha magonjwa  ya kiharusi, kisukari na ugonjwa wa moyo.
 
Kabohaidreti (wanga) kwa wingi au vyakula vyenye sukari kupitiliza
Kundi hili ndilo ambalo watu wengi hulichanganya kwa kuamini kuwa tambi ‘supagheti’ ni chakula chepesi kuliwa usiku, kitu ambacho si sahihi.
Tambi ni moja ya vyakula ambavyo havipaswi kuliwa usiku kwani ina wanga mwingi ambao kutokana na kulala hakisagiki na kinaweza kuziba mirija ya damu na kusababisha madhara kwa mtumiaji.
Kipande kidogo cha keki kinaweza kuwa kizuri kwa mtumiaji, lakini akizidisha siyo nzuri kutokana na kuwa na sukari nyingi. Vilevile mkate mweupe uepukwe una wanga mwingi.
Nyama nyekundu na vyakula vyenye protini nyingi
Kula nyama nyekundu usiku kunamfanya mhusika asipate usingizi mzuri kwa kuwa tumbo linashindwa kusaga vyakula vigumu uwapo usingizini.
Kama ni lazima  kula nyama, basi ni vyema ikawa ni nyama nyeupe kama vile kuku na samaki na kuepuka vyakula vyenye protini. Ikishindikana, basi  glasi ya maziwa ya moto inaweza kukidhi haja bila kuwa na madhara.

Vyakula vyenye viungo vingi
Hupaswi kula vyakula vya aina hii kwa kuwa vina kemikali ambayo inaweza kukukosesha usingizi.
Kahawa
Kwa kawaida, kahawa ina kafeini ambayo inaweza kusababisha usumbufu wakati wa kulala kwani hata dawa zenye kafeini hapaswi kupewa mgonjwa mwenye matatizo ya kulala.
Vivyo hivyo, kwa asiyekuwa mgonjwa ina madhara pia hapa hata soda ambazo zina kafeini, pia zinasababisha mtumiaji kukosa usingizi wa kutosha, hivyo kushindwa kufanya mambo katika mpangilio maalumu siku inayofuata.
Wataalamu  wa masuala ya chakula na lishe, Wanasema kuwa kama ni lazima kunywa kahawa, basi iwe ni saa tano au nne kabla ya kwenda kulala.
wanasema kuwa kuna baadhi ya vitu vina madhara kwa mtumiaji bila kujua kutokana na kuwa na mazoea ya kutumia kitu hicho ambapo matokeo yake madhara yake huwa ni mhusika kupata tatizo la kukosa usingizi.
Kula chakula kingi
Madhara ya kula chakula kingi ni mengi, mojawapo ni kukosa usingizi kutokana na kushiba kupita kiasi.
Athari za kufanya hivi ni pamoja na kuukosesha mwili uwezo wa kusaga chakula kwa kuwa utakuwa umeshiba sana na mwili umepumzika.
“Ukiwa katika hali hii hata usingizi unakuwa ni wa shaka kwa kuwa unakuwa umeshiba sana, lakini hicho chakula hakifanyi kazi ipasavyo na ndiyo maana ni rahisi kuongezeka uzito, hakimeng’enyeki kwa urahisi,”
Vyakula vilivyokaangwa
Vyakula hivi husababisha kiu, hivyo humlazimu mtumiaji kunywa maji mengi na kumlazimisha kwenda msalani mara kwa mara.
 Mwili unahitaji kupumzika kwa kulala kwa saa sita hadi nane ili ufanye kazi na mhusika akiamka aanze upya.
“Kikubwa hapa ni kupunguza kula vyakula ambavyo vitahitaji maji au vyenye maji maji kuepuka kwenda msalani mara kwa mara au kuamka.
 
Pombe
Kunywa pombe saa chache kabla ya kulala au kunywa na kulala huku ukiwa nazo kichwani hata kama hujalewa siyo nzuri kiafya kwa kuwa huufanya mwili kulala kama mzigo hivyo inakuwa siyo kupumzika bali kulazimika kulala kwa ulevi.
 
Mtaalamu mmoja wa lishe anasema kuwa mwili unahitaji kupumzika ukiwa huru na siyo kulazimishwa na kilevi, kwani kupumzika ni pamoja na kufahamu sasa naenda kupumzika na mwili unauandaa kwa ajili hiyo, lakini ukiwa umelewa hali kama hiyo haipo.
Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Ndani (Mfumo wa Chakula), Dk Raymond Mwenesano wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) anasema kuwa kwa kawaida mwili wa binadamu unapohitaji mapumziko au unapofika muda wa  kupumzika inabidi uwe huru kwa maana ya kuwa katika hali ya kawaida, hususan sehemu za ndani kama tumbo.
Anasema kuwa kama utapumzika huku ukiwa na vitu vya ziada ambavyo vitakuwa na usumbufu kwako kama kushiba, kulewa unakosa ile dhana nzima ya kupumzika na matokeo yake ni kutimiza wajibu wa kulala na si kulala kwa ajili ya kupata mapumziko.
Mariam Rashid, ambaye ni mnene kiwajihi anasema kuwa tangu aanze kupunguza kula vyakula vyenye wanga wakati wa usiku amepungua uzito kwani alikuwa ni lazima ale wali au chapati usiku na kujikuta ana uzito mkubwa akashauriwa na daktari kupunguza uzito na kwa kuanza alianza kupunguza kula na kushiba usiku ikiwemo kuacha vyakula vyenye wanga.
“Nakula matunda na mboga mboga kabla ya kulala na huu ni ushauri niliopewa na daktari wakati ambapo nilikuwa na uzito mkubwa ilikuwa karibu kilo 70 wakati urefu wangu ni futi tano, ilikuwa ni hatari na daktari alinikemea na kunitaka nipungue kwa kuwa nilikuwa nimeshaanza kupata tatizo la miguu na kukosa usingizi,” anasema.
Mtaalamu wa masuala ya Saikolojia wa Chuo Kikuu cha Dodoma, Modesta Kamongi amesema kuwa si tu unene unaohatarisha afya ya mhusika, bali pia humfanya asijiamini.
Anasema ni vyema kila mmoja akawa na mwili wa wastani kwani mara nyingi wamekuwa wakipata malalamiko kwa watu wanene hujichukia na kutaka wapatiwe ushauri wa jinsi ya kukabiliana na wale wanaowatania.

3 comments:

  1. ah somo liko vizur tuendelee na kutuelumisha

    ReplyDelete
  2. Sas ni chakul kipi kinafaa kula wakati wa usiku?

    ReplyDelete
  3. mbayabzaid ndo vyakula vinavyopatikana kwa wepesi zaid kwa hapa mjini sasa duuuh....ila somo limeeleweka.

    ReplyDelete