INZI wa kijani anayefahamika kwa jina la kitalaamu kama Lucilia Sericata (green bottle fly) ni kati ya wadudu wanaoogopwa na binadamu kwa sababu ni chanzo cha ugonjwa wa kipindupindu na magonjwa mengine ya kuhara.
Kuogopwa huko kunatokana na ukweli kuwa nzi hao tofauti na wadudu wengine hupenda kuishi katika mazingira machafu kama vyooni, kwenye mizoga ya wanyama na mashimo ya taka.

Hofu ya binadamu kuhusu mdudu huyo unaweza kuitambua anapopita karibu na meza ya watu wanapokula nyumbani au hotelini. Baadhi wanaweza hata kukosa hamu ya kuendelea kula.

Lakini mtazamo kuhusu mdudu huyo ni tofauti kwa wanasayansi wa Taasisi ya Utaifi wa Kilimo (KARI) ya nchini Kenya, hasa baada ya kuanza kuwatumia funza wanaotokana na nzi hao katika utafiti wa tiba ya vidonda sugu, visivyopona kwa dawa ya antibiotic.
Utafiti huo unaendelea katika Hospitali ya Kenyatta na kwa mujibu wa Dk. Phoebe Mukiria ambaye anasimamia utafiti huo, mwenendo wa utafiti wa tiba hiyo umefikia hatua nzuri.

Dk. Mukiria anaeleza kuwa kimsingi tiba hiyo ya kutumia funza wanatokana na nzi wa kijani si ngeni na ilikwishawahi kutumika katika nchi zilizoendelea kama Marekani na nchi za Ulaya katika miaka ya zamani.

Hatua ya kwanza
Kwa mujibu wa mwanasayansi huyo hatua ya kwanza katika tiba hiyo ni ile ya kuweka nyama iliyooza au chakula katika sehemu ya wazi ili kuwavutia nzi wa kijani katika eneo hilo.
“Kutokana na harufu mbaya ya nyama, nzi wa kijani huanza kujaa eneo hilo nasi tunawatega kwa kutumia wavu maalumu na baada ya hapo tunawahifadhi katika chombo chenye wavu (cages),” anaeleza.
Baada ya hatua hiyo nzi hao huanza kutaga mayai ambayo baada ya siku tano hugeuka kuwa funza kabla ya kuanza hatua ya kufikia au kuzaliwa nzi mwingine.

“Baada ya hatua hiyo ndipo tunawachukua funza hao na kuwaosha vizuri kwa maji ya uvuguvugu kisha tunaweka katika vyombo maalumu (container) na kisha tunawasafirisha hadi Hospitali ya Kenyatta kwa ajili ya tiba kwa wagonjwa,” anasema mtaalamu huyo.

Anaeleza zaidi kuwa katika hospitali hiyo madaktari wanaotibu wagonjwa wenye vidonda vikubwa ambavyo ni sugu, huwatumia funza hao kwa kuwafunga katika sehemu yenye kidonda katika mwili wa mgonjwa, kwa kutumia bandeji yenye matundu ya kuingiza hewa.
“Kwa kawaida funza hujilisha katika tishu za mwili zilizokufa (dead tissue) na hatua hiyo hufanya kidonda kuwa kisafi na tishu zilizohai kuanza kupona”

“Pia funza wana midomo kama sindano ambayo husaidia kufyonza uchafu ulioko katika kidonda hasa usaha na madaktari huwabadilisha funza kila baada ya siku mbili au tatu katika kidonda,” anasema daktari huyo.
Lakini anawatoa hofu wagonjwa na watu wanaotilia shaka tiba hiyo akisema; “Si rahisi funza wazaliane katika kidonda kwa sababu kwa kawaida funza hujilisha kwenye tishu za mwili zilizokufa na uchafu unaozalishwa katika kidonda na si vinginevyo.

Dk. Mukiri anasema, pamoja na watalaamu wenzake, wanashukuru tiba hiyo kuwa suluhu ya vidonda sugu na tayari mafaniko yake yameleta matunda kwa baadhi ya wagonjwa ambao wamepona vidonda vyao.
“Bado utafiti zaidi unaendelea lakini niseme tu kwamba tayari baadhi ya wagonjwa waliotibiwa kwa njia hiyo wamepona vidonda vyao na wengine wameonyesha maendeleo makubwa,”anasema Dk. Mukiri.

Changamoto za tiba hiyo
Kwa mujibu wa mwanasayansi huyo changamoto kubwa ya tiba hiyo ni ile ya wagonjwa na ndugu zao kukataa aina hiyo ya tiba ambayo wengine wanaona kuwa ni ya “aibu”.
“Wagonjwa wengine na ndugu zao wanaowauguza wamekuwa wakikataa aina hii ya tiba, wakidhani kuwekewa funza katika kidonda ni tiba ya aibu hivyo kuwapa madaktari wakati mgumu katika kuwashawishi,” anaeleza Dk. Mukiri.
Anasema kwa kawaida madaktari hawana mamlaka yoyote katika tiba hii kwa kuwa bado iko katika majaribio, hivyo wanalazimika kwanza kupata ridhaa ya mgonjwa mwenyewe na ndugu zake kabla ya kufanyiwa matibabu hayo.
Dk. Kimani Wanjeri wa Hospitali ya Kenyatta ni miongoni mwa jopo la watalaamu wa tiba wanaosimamia majaribio hayo ambaye anaeleza kuwa njia hiyo ya tiba inaweza kuwa mkombozi kwa wagonjwa wenye vidonda sugu ambavyo haviponi kwa kutumia dawa zaantibiotics.

“Tiba hii pia haina maumivu kwa wagonjwa na ni rahisi zaidi kwa upande wa gharama kwa wagonjwa na ndugu zao, hupunguza muda wa wagonjwa kukaa hospitalini, ”anaeleza.
Daktari huyo anasema mzunguko wa funza katika kidonda hufanya damu katika eneo lenye jeraha kuwa rahisi zaidi na kurahisisha hatua ya kuelekea kupona kwa kidonda.

Anaeleza zaidi kuwa baada ya tiba hiyo kuna vidonda vina pona kabisa na vingine huendelea kutibiwa zaidi ikiwa pamoja na kufanyiwa upasuaji mdogo (grafting).
Nchi nyingine ambazo zinatajwa kuwa tiba hiyo imekuwa ikitumika ni pamoja na Marekani na Afrika ya Kusini.