Saturday 3 May 2014

UGONJWA WA UPUNGUFU WA DAMU (ANAEMIA)



Anaemia au upungufu wa damu ambao umekuwa tatizo kwa jamiii mbalimbali ulimwenguni, hususan katika nchi zetu za Kiafrika Tanzania ikiwa miongoni mwao.

Anaemia ni jina jumla linalotumiwa kubainisha aina mbalimbali za upungufu wa damu mwilini.

VIPI INATOKEA?
Upungufu huo wa damu hutokea iwapo ukolezi au mkusanyiko wa pamoja wa chembe nyekundu za damu (haemoglobin) vinapopungua kupita kiwango cha kawaida.

 
Kwa ufupi Anaemia husababishwa na mambo makuu matatu yafuatayo:
1. kupoteza damu, kwa mfano kunakotokana na vipindi vya hedhi inayotoka kwa wingi sana au kuvuja damu kunakosababishwa na vidonda vya tumbo au ulcers.
2. uzalishwaji duni wa chembe nyekundu za damu unaosababishwa na upungufu wa vitamini au lishe duni na vile vile magonjwa sugu au ya muda mrefu ambapo bone marrow huwa haifanyi kazi ipasavyo.
3. kuharibiwa kwa chembe nyekundu za damu kunakosababishwa na magonjwa ya kurithi (hereditary), magonjwa kama vile kansa au athari mbaya zinazotokana na utumiaji wa baadhi ya dawa. 

DALILI ZA UGONJWA HUU.
Dalili za Anaemia au upungufu wa damu ni zipi
Mtu mwenye tatizo la upungufu wa damu mara nyingi huwa amepauka mwili na huwa na dalili zifuatazo:

 
 1. hujisikia kuchoka.
2. dhaifu na huwa na mwendo kasi wa damu (yaani high pulse rate).
3. huhisi kiu,
4. kizunguzungu wakati akisimama
5. Huhema na kuwa na mpapatiko wa moyo wakati akitumia nguvu. 

Kuna aina mbalimbali za Upungufu wa Damu au Anaeamia. Kwanza ni:
1. Iron defiency anaemia (Huu ni upungufu wa damu anaopata mtu wakati anapopoteza kiwango fulani cha madini ya chuma mwilini.
Itafahamika kuwa mwili wa wanadamu unahitaji madini ya chuma ili kuweza kuzalisha chembe nyekundu za damu. Na vile vile itakumbukwa kuwa, iwapo mtu atapoteza kiasi fulani cha damu, madini ya chuma nayo hupungua mwilini na hivyo kusababisha upungufu wa madini hayo kwa muda.
Ulaji wa madini ya chuma katika mlo wa kawaida wa mtu hauwezi kufidia kiwango cha madini kilichopotea, kwa hiyo akiba ndogo iliyobakia mwilini ya chuma hutumika mara moja. Kwa hakika upungufu wa damu unaosababishwa na ukosefu wa madini ya chuma au Iron deficiency anaemia, huathiri watu wengi duniani.

JE, UPUNGUFU HUU WA DAMU HUWAPATA AKINA NANI ZAIDI?.

Kwanza ni wanawake ambao wako katika umri wa uzazi (kwa sababu hupoteza damu wakati wakiwa katika hedhi zao).
Pili wanawake wajawazito (kwa kwa kuwa madini ya chuma waliyonayo hutumiwa na viumbe vilivyoko kwenye matumbo yao kabla ya kuzaliiwa),
Tatu, ni watoto wanaonyosha maziwa, ambao huanza kula mlo kamili. Katika kipindi hiki cha ukuaji wa mtoto, akiba ya madini ya chuma ya mtoto aliyoipata kutoka kwa mama, huanza kupungua, kwa hivyo maziwa anayonyonya huwenda yakawa hayana chuma ya kutosha.

Aina nyingine ya upungufu wa damu ni Haemolytic Anaemia: Katika aina hii ya Anaemia chembe nyekundu za damu huharibiwa haraka kuliko mwili unavyoweza kuzalisha chembe nyingine. Upungufu huu husababishwa na mambo mengi lakini hapa ninataja baadhi tu kama kansa aina ya lymphoma au utumiaji wa baadhi ya dawa ambazo huweza kuangamiza chembe nyekundu za damu kwa mfano dawa aina ya methylodopa.
Nukta ya kuzingatia hapa ni kuwa, baadhi ya dalili za ugonjwa huu ni hizi zifuatazo:
Homa, kutetemeka kwa mwili,
maumivu ya tumbo na mgongo na kushuka ghafla kwa mapigo ya moyo.
Aina nyingine ni ile inayoitwa Pernicious anaemia. Huu ni upungufu wa damu unaotokana na ukosefu wa kutosha wa acidi aina ya folic (folate) katika chakula.
Folate hupatikana katika mbogamboga za rangi ya kijani, matunda na nyama. Kwa kuzingatia kuwa mwili huhifadhi kiasi kidogo cha asidi ya folate, mtu ambaye hali kwa wingi vyakula vya aina hiyo anaweza kukabiliwa na tatizo hilo katika kipindi cha miezi michache.
BILA SHAKA MSOMAJI UTAPENDA KUULIZA SWALI KWAMBA VIPI
tunaweza kukabiliana na tatizo hili?
Jibu ni rahisi kabisa, kwanza hakikisha kuwa chakula unachokula kina aina zote za vyakula vilivyovitaja na vile vile iwapo italazimu, unaweza kutumia dawa za kuongeza madini hayo. 

Aina nyingine ni Aplastica Anaemia.
Huu ni upungufu wa damu unaotokea wakati bone marrow zinaposhindwa kuzalisha chembe nyekundu za damu ipasavyo. Baadhi ya upungufu huu wa damu humpata mtu anapotumia tiba ya miale (radio therapy) au dawa za saratani na kemikali nyinginezo.

Aina nyingin ni Sickle cell Anaemia:
ni upungufu wa damu ambao chembe nyekundu za damu huwa na muundo usio wa kawaida unaozuia na kuathiri mishipa midogo ya damu na hivyo kusababisha kuziba kwa mishipa hiyo ya damu na hata kiungo cha mwili. Sickle cell anaemia huwaathiri sana watu weusi. 

Kwa msingi huo ni muhimu kwa mtu kujua aina ipi ya upungufu wa damu aliyonayona na hilo hujulikana baada ya daktari kukuandikia vipimo kadhaa vya damu ambavyo vitaonyesha unakabiliwa na aina ipi ya Anaemia. 

 
 Uzuiaji na Matibabu
Njia za kuzuia na kutibu aina zote hizi za upungufu wa damu zitategemea unakabiliwa na aina gani kati ya hizo.
Kwa hiyo matibabu yatafuata kulingana na aina ya upungufu wa damu ulionao.
Hata hivyo tunakumbusha kuwa, katika aina nyingine za anaemia, lishe na matibabu tu hayatoshi kumponyesha mtu. Kwa hivyo daktari atashauri mtu aongezwe damu mwilini.

0 comments:

Post a Comment