Friday 11 July 2014

LISHE KWA MGONJWA WA KISUKARI





LEO tunaendelea tena kuangalia suala la lishe kwa wagonjwa na hapa tunamuangalia mgonjwa wa kisukari. Kama tulivyokwisha ona katika makala nyingine zilizopita, mgonjwa yeyote wa magonjwa hatari kama presha, moyo, saratani, kisukari n.k, ni lazima ajue vyakula anavyopaswa kula au kutokula.
Elimu ya lishe ni muhimu sana, kwani madhara ya ugonjwa huonekana haraka na hata kusababisha kifo upesi, iwapo mtu ataendelea kula bila kujijua vyakula vilevile vilivyosababisha tatizo la kiafya alilonalo.
Kwa ujumla, mgonjwa wa kisukari (Diabetic), hana mipaka mingi ya vyakula, anaweza kuendelea kula vyakula vingi kama kawaida iwapo atajua jinsi ya kula, kiasi gani na kwa wakati gani. Hata hivyo, kama ulaji wake ulikuwa hauzingatii ulaji sahihi, baada ya kuugua hana hiyari bali kufuata kanuni za ulaji sahihi.
Kanuni kuu ya ulaji anayopaswa kuzingatia mgonjwa wa kisukari ni kula kiasi bila kushiba sana, kula kwa muda uleule kila siku, na kula mchanganyiko wa matunda, mboga na nafaka zisizokobolewa. Hii ina maana kwamba mgonjwa anatakiwa asisikie njaa wala shibe muda wote wa siku.

KITU GANI UNAKULA?
Bila kujali kama una kisukari au la, afya bora iko mikononi mwako kwa kuwa na hiyari ya kuchagua unachokula. Lakini unapokuwa tayari mgonjwa, unakuwa huna hiyari tena ya kuacha kuzingatia ulaji sahihi, vinginevyo unakiita kifo haraka. Kimsingi, mgonjwa wa kisukari azingatie zaidi ulaji wa vyakula vitokanavyo na mimea, aache kula vyakula vya kusindika, vyenye sukari na mafuta mengi.
WAKATI GANI WA KULA?
Suala la kujali muda wa kula kwa mgonjwa wa kisukari ni la lazima, kwa sababu atatakiwa wakati wote kudumisha kiwango cha sukari mwilini mwake kwa kula kwa wakati uleule ili kuepuka kusikia njaa ambayo husababisha sukari kushuka kwa kasi.

KIASI GANI UNAKULA?
Vilevile suala la kula kiasi kwa mgonjwa wa kisukari si la hiyari tena, bali ni la lazima. Hata mtu akila vyakula bora vyenye virutubisho vya hali ya juu kiasi gani, kama akivila kupita kiasi huweza kusababisha unene ambao ni sababu moja wapo ya ugonjwa wa kisukari, hivyo ni muhimu kuzingatia kiasi.
Mgonjwa wa kisukari hahitaji kuwa na chakula maalumu, bali anatakiwa kutilia maanani ulaji wa mboga, matunda na nafaka zisizokobolewa. Lishe ya mgonjwa wa kisukari ni ya kawaida tu yenye vyakula vyenye virutubisho vingi na mafuta kidogo na kiasi kidogo cha wanga.

ZINGATIA
Mgonjwa wa kisukari anashauriwa kula matunda, lakini anakatazwa kunywa juisi za matunda. Halikadhalika, matunda kama ‘Apples’, ‘Peas’ na mengine ya jamii hiyo, ni bora yaliwe pamoja na maganda yake.
Miongoni mwa matunda bora kabisa kwa mgonjwa wa kisukari ni zababi mbivu, hizi zikiliwa kila siku mara tatu kwa siku, huweza kuwa tiba kabisa ya kisukari.
Halikadhalika majani ya embe nayo ni dawa ya kisukari. Loweka majani mabichi ya mwembe, kiasi cha kiganja kimoja (gramu 15), kwenye nusu lita ya maji usiku kucha, kisha asubuhi yakamue upate maji yake, kunywa kila siku asubuhi na unaweza kukidhibiti kisukari, hasa kile kinachopanda nyakati za asubuhi.

0 comments:

Post a Comment